08/03/2026
Wanawake wa Taasisi ya Saratani Ocean Road wameungana na wanawake wengine kuadhimisha siku ya wanawake duniani leo Machi 8, 2026 katika viwanja vya Barafu Mburahati jijini Dar es Salaam, wakilenga kuhamasisha haki na usawa kwa wanawake na wasichana.
Maadhimisho haya yaliyoongonzwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar-es-Salaam Mhe. Arbelt Chalamila yamehudhuriwa na mamia ya wanawake kutoka taasisi mbalimbali za umma na binafsi, vikundi vya kijamii pamoja na wadau wa maendeleo, kwa lengo la kusherehekea mafanikio ya wanawake na kujadili namna ya kuimarisha usawa wa kijinsia katika jamii.
Akizungumza katikq maadhimisho hayo, mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila amewasisitiza wanawake juu ya umuhimu wa kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya taifa huku akiwataka kuendelea kujitokeza katika nafasi mbalimbali za uongozi na kutumia fursa zilizopo kuboresha maisha yao na ya jamii inayowazunguka.
Maadhimisho haya yamefanyika chini ya kauli mbiu isemayo, "Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050” inayohamasisha wanawake kushiriki kikamilifu katika shughuli za uongozi na maendeleo ya kijamii na kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuendelea kupaza sauti ya usawa na haki kwa wanawake.
Maadhimisho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha wanawake na wadau mbalimbali ili kujadili changamoto zinazowakabili pamoja na kuweka mikakati ya kuimarisha afya, ustawi na maendeleo ya wanawake nchini.
HERI YA SIKUKUU YA WANAWAKE DUNIANI....